Dereva Aliyetoa Rushwa ya Elfu 5 Kwa Trafiiki Naye Asakwa Na Jeshi La Polisi



Jeshi  la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limesema linamsaka dereva aliyempa rushwa ya Sh. 5,000 askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani ambaye amefukuzwa kazi, kwa ajili ya kukamilisha upelelezi.
 
Katikati ya wiki, video fupi iliyokuwa ikionyesha askari huyo akipewa rushwa na dereva wa gari ndogo ilisambaa kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii na kusababisha Polisi kumchukulia hatua trafiki huyo.

Kamanda wa Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa, aliwaeleza waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam "video ile" iliwashutua na walichukua hatua mara moja za kumfukuza kazi na sasa ni raia wa kawaida.

Juzi Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Kamishna Msaidizi wa Polisi Jumanne Murilo, alisema askari huyo alifukuzwa tangu Jumanne.

Kamanda Murilo alisema askari huyo hadi anafukuzwa kazi ndani ya Jeshi la Polisi alikuwa amefanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja na nusu.

"Tukio hili lilifanyika eneo la Mwenge na baada ya kulibaini tulianza uchunguzi wetu ambao juzi (Jumanne) ulikamilika na kubaini tukio hilo lilikuwa la kweli (kwamba) amepokea rushwa. Hivyo tumemuondoa kazini," alisema juzi Kamanda Murilo.
 
Kamanda Murilo ambaye hakumtaja jina askari huyo aliwakumbusha trafiki kuzingatia maadili ya kazi na taratibu za kijeshi zilizowekwa.

Akirejea taarifa hizo, Mambosasa alisema upelelezi wa shauri hilo unaendelea .

"Kwa sasa upelelezi unaendelea ili kumfikisha mahakamani mtuhumiwa ambaye kwa sasa si askari tena," alisema Kamanda Mambosasa.

"Lakini kama ambavyo sheria za rushwa zinavyoelekeza ni lazima tumpate na aliyehusika kutoa rushwa ili kupata ushahidi wa kesi hiyo," alisema Mambosasa.

Alieleza zaidi kuwa ingawa wanamsaka mtuhumiwa huyo namba mbili, pia wanamshukuru kwa ushirikianao uliowezesha kupatikana kwa askari huyo na hatua kuchukuliwa dhidi yake.

"Badala ya raia kulalamika na kusema Jeshi la Polisi halifanyi kazi ni vyema mkatoa taarifa kama alivyotoa huyu aliyerekodi video, aliyewezesha kumnasa aliyekuwa askari wetu na tukambaini kweli na kosa la kuomba rushwa ya Sh. 5,000 wakati serikali inapambana na matukio kama hayo," alisema.

Katika tukio hilo, dereva aliyeombwa rushwa alimrekodi askari huyo kupitia simu ya mkononi wakati akimpatia rushwa hiyo iliyowekwa chini ya leseni.

Post a Comment

[blogger]

MKRdezign

Blogger Widgets

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget